Feb 19, 2013

HIZI NI KAULI ZA SERIKALI YA ZNZ NA MAASKOFU WAKUU KATOLIKI KUHUSU MAUAJI YA PADRE.



.
Baada ya kifo cha Padre Evarist Mushi ambae alifariki kwa kupigwa risasi Zanzibar jumapili iliyopita, kanisa Katoliki limewataka waumini wa kanisa hilo na Watanzania wengine kuwa watulivu na kufanya maombi ya amani katika kipindi hiki.
Askofu mkuu wa kanisa hilo Tanzania Muadhama Polycarp Cardinal Pengo amesema kifo cha Padre Mushi ni pigo kwa kanisa na Taifa na ni ishara ya kutoweka kwa amani hivyo hilo swala linatakiwa kufanyiwa kazi kabla ya madhara kuzidi, kwa sababu ukikosekana usalama kwa imani moja, kesho na kesho kutwa haijulikani ni imani gani ikashambuliwa.
Namkariri akisema “vyombo vya usalama vinatakiwa viwe makini, mimi sio mtaalamu wa usalama lakini naona ni jambo ambalo lingeweza kuzuilika na lisitokee kama watu wangesoma ishara za nyakati, wale wanaohusika wazuie kisitokee chochote… kuendeleza moyo wa kisasi hakutasaidia chochote na badala yake kutaleta madhara zaidi”
Padre Evarist Mushi atazikwa february 20 2013 huko Zanzibar ambapo pia misa kubwa ya kuomba amani imepangwa kufanyika siku hiyohiyo kwenye kanisa la Mtakatifu Joseph jijini Dar es salaam.
Kwenye sentensi nyingine ni kwamba Serikali ya Mapinduzi Znz imewaondoa hofu wananchi wake kuhusu ujio wa makachero kutoka nje ya nchi kwani umelenga kuliangamiza kundi lenye mtandao wa kihalifu linalotishia amani ya Zanzibar na Tanzania.

.
Waziri wa nchi ofisi ya makamu wa pili wa Rais Zanzibar Mohamed Aboud amesema Serikali imekerwa na matukio ya kushambuliwa kwa viongozi wa dini, matukio ambayo yanaendelea kutokea ndio maana inaamini uamuzi wa kuwatumia makachero kutoka nje ya Tanzania utasaidia kuumaliza mtandao unaofanya uhalifu huo.
Namkariri akisema “Wenzetu hawa wa mataifa makubwa wameendelea sana na wamefanya mambo haya kwa muda mrefu, inastaajabisha sana kwa mtu wa Zanzibar kutokea akaenda kumpinga risasi mtu asie na hatia, haijawahi kutokea mtindo huu
Askofu wa kanisa katoliki Znz Agostino Shao amesema “kuna watu ambao wamepandikizwa tayari na wanakuja kwa mwamvuli wa dini ya kiislam, sasa hao ndio wanaharibu Uislamu wetu na hao wengine ndio wanaoharibu dini yetu ya kikristo pia, sidhani kama haya yanayofanyika Znz yameundiwa hapahapa kwa sababu ukimuuliza Mzanzibar yeyote hata Rais anasema mimi nimesoma Mission, karibu wote wamesoma shule za Mission… “
Kwenye mstari mwingine Askofu Shao amesema “hii ni shida inayopandikizwa na watu wenye njia mbaya maana ukishasema Waislamu unamjumuisha na hata mama mzee, kibibi kilichoishi kwa miaka yote hiyo Uislamu wake mzuri, Wazee wetu wameishi Uislamu wao mzuri wakichanganyika na wengine leo ndio mnasema ndio analete fujo hataki kuishi na Wakristo, mimi nisingependa kusema ni Waislamu wote kwa ujumla wanahusika, katika kila dini kuna watu wazuri na Waovu, baadhi ya Waislamu ambao wana sera zao za tofauti na dini hii ya Kiislam ndio wanaweza kuwa watendaji, baadhi ya Wakristo ambao wana siri zao za dini yao ndio wanaweza kuwa watendaji, lakini ukisema Waislamu wote nitakataa”

No comments: