Feb 25, 2013

‘Bajeti ya kilimo itafikia asilimia 10’


 
Na  Suzan Mwillo  (email the author)

Posted  Jumatatu,Februari25  2013  saa 19:32 PM
Kwa ufupi
“Hii ni fursa mzuri kwetu kujifunza mambo mengi yatakayotuwezesha kufanya maboresho kwenye kilimo,” alisema waziri huyo.
 

WAZIRI wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza, ameelezea matumaini yake kuwa bajeti ya kilimo itaongezeka kutoka asilimia saba ya sasa hadi kufikia asilimia 10 ifikapo mwaka 2015.

Chiza aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza katika mkutano wa Kuimarisha Kilimo kwa Lishe Bora inaojumuisha mataifa 18 ya Afrika Mashariki na Kati.

Mkutano huo wa siku nne, utatoa fursa kwa washiriki, kutambua umuhimu wa sekta ya kilimo na jinsi ya kuboresha miundombinu yake.

Waziri huyo alisema Serikali inatambua kuwa kilimo ni sekta muhimu na inayochangia kwa asilimia kubwa, kukuza pato la nchi chakula kwa ajili ya matumizi ya wananchi.
Alisema kwa msingi huo, itaendelea kuipa kipaumbele sekta hiyo kwa kuitengea fedha za kutosha, ili iweze kuleta tija zaidi.

Chiza alisema mkutano huo unafanyika Tanzania kwa sababu ni moja kati ya nchi zilizotia saini mpango wa uwekezaji katika kilimo.

“Hii ni fursa mzuri kwetu kujifunza mambo mengi yatakayotuwezesha kufanya maboresho kwenye kilimo,” alisema waziri huyo.

Alisema mkutano huo utasaidia kuibua mijadala itakayotoa dira ya namna ya kukabiliana na chanagamoto katika sekta ya kilimo.

Katika hotuba yake, waziri huyo alisema mwaka huu taifa linakabiliwa na upungufu wa chakula uliosababisha na upungufu wa mvua katika baadhi ya mikoa.
Alisema hata hivyo kuna matumaini kuwa hali ya chakula nchini itaimarika katika miezi kadhaa ijayo.

No comments: