Jun 8, 2013

WAASI WA M23 WAKUBALI KUREJEA KATIKA MAZUNGUMZO YA AMANI NA SERIKALI


Kiongozi wa kundi la M23 Bertrand Bisimwa Photo AFP / Isaac Kasamani
 
Kundi la waasi la M23 la nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC linarejea katika mazungumzo ya amani na serikali ya Kinshasa mwishoni mwa juma hili mazungumzo ambayo serikali ya nchi hiyo inaona kuwa ni jambo sahihi katika utatuzi wa mgogoro huo.

M23 chini ya kiongozi wake Bertrand Bisimwa walitangaza uamuzi huo kwa kile walichosema ni kutokana na wito wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon na Mjumbe wake katika mataifa ya ukanda wa maziwa makuu kuwa suluhu ya mgogoro huo itapatikana kwa njia ya mazungumzo.

Taarifa ya M23 iliyotolewa juma hili ilibainisha kuwa Rene Abandi ndiye atakayeongoza ujumbe huo wa M23 kuelekea Kampala.

Mashirika ya kiraia Mashariki mwa nchi hiyo yanaendelea kuhofia jitihada za waasi hao ambao wanasemekana kuwa wamekuwa wakipanga kuuchukua mji wa Goma uliopo Mashariki mwa nchi hiyo.

Awamu ya mwisho ya mazungumzo ya amani kati ya serikali ya DRC na waasi wa M23 yalivunjika mwezi Aprili mwaka huu.

No comments: