Jun 30, 2013

SERIKALI YASHUSHA USHURU WA PETROLI....USHURU WA SIMU WAFUTWA



MFUMO mpya wa Bunge kuanza na bajeti za kisekta na kumalizia na Bajeti ya Serikali pamoja na uundwaji wa Kamati ya Bajeti, umeonesha makali yake kiasi na kuilazimisha Serikali, kushusha kodi ya petroli na kufuta ushuru wa kutuma na kupokea fedha kwa njia ya simu.


Kabla ya Serikali kufikia uamuzi huo jana saa sita usiku, Kamati ya Bunge na wabunge walivutana na Serikali mara kadha wa kadha juu ya kodi mbalimbali, na kulazimika Kamati hiyo na Serikali kukaa si chini ya mara mbili, kujadili.
Katika vikao vyao, vikao viwili vya juzi na jana, Kamati ya Bajeti inayoongozwa na Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge (CCM), na Waziri wa Fedha, William Mgimwa, naibu wake wawili na wataalamu wake wa wizarani, walikaa kujadili tofauti zao mpaka saa sita usiku.


Mvutano wa Kwanza Mvutano wa kwanza ulianza mwanzoni mwa wiki hii, baada ya Waziri Mgimwa kuanza kujibu hoja za wabunge kuhusu Bajeti ya Serikali, ambayo ilipongezwa na kupingwa na Kamati ya Bajeti.


Hoja za wabunge na Kamati ya Bajeti, zilihusu punguzo la kodi katika mishahara, petroli, huduma za simu na magari yenye umri wa kuanzia miaka 10 na kuendelea na kodi katika huduma za utalii.


Hata hivyo, Mgimwa alipokuwa akijibu hoja za wabunge kabla ya kuwaomba wapitishe Bajeti ya Serikali, aliwataka wapitishe kwanza bajeti hiyo na hizo hoja zao zijibiwe katika Muswada wa Sheria ya Fedha, hatua ambayo wabunge waliiridhia na Bajeti ya Sh trilioni 18.2, ikapita.


Hata hivyo baada ya Bajeti kupita, Mgimwa aliwasilisha Muswada huo, ambao uliacha baadhi ya kodi ikiwemo ya magari mabovu kuzidi miaka 10, ya petroli na dizeli na ya simu.


Baada ya Mgimwa kumaliza kusoma Muswada huo, Chenge huku akiungwa mkono na wabunge wengi, alipokuwa akisoma maoni ya Kamati ya Bajeti, alisisitiza baadhi ya kodi zifutwe au kupunguzwa na kuielekeza Serikali kutafuta vyanzo vipya katika ripoti ya Kamati ya Spika ya vyanzo mbadala vya mapato ya Serikali.


Vikao vya saa sita usiku Kutokana na mvutano huo, Waziri wa Fedha na Kamati ya Bajeti walikutana Jumatano wiki hii mpaka saa sita usiku na hata walipotoka, walikuwa hawajaafikiana, kiasi cha Mgimwa kuja na marekebisho kidogo, ikiwemo kuondoa kodi ya utalii, lakini Chenge akaja na msimamo katika kodi ya petroli na utumaji na upokeaji fedha kwa njia ya simu.

Baada ya maoni ya Chenge, wabunge saba walileta majedwali ya mabadiliko, na kusababisha Spika wa Bunge, Anne Makinda, kuitaka Kamati ya Bajeti, Waziri wa Fedha na hao wabunge kurudi kutafuta suluhu juzi.

Katika kikao hicho cha suluhu cha juzi Alhamisi, Kamati hiyo na Waziri, waliendelea kuvutana mpaka saa sita usiku tena ndipo wakaafikiana, ambapo jana walikuja na kauli moja.


*Suluhu
Kabla ya Mgimwa kutangaza mwafaka, Chenge alipewa nafasi na kumsifu Waziri Mgimwa kwa kuwa msikivu na mtu asiyependa makuu na kusema, wamefikia makubaliano ambayo ni habari njema kwa Watanzania.

Baada ya Chenge kutangaza habari hiyo njema, Mgimwa alisimama na kuanza na kodi ya petroli, ambapo alisema Serikali imeridhia kutoongeza ushuru wa bidhaa katika petroli wa Sh 61 na hivyo, itaendelea na ushuru uliopo wa Sh 333.

Alisema pia wameridhia kusitisha kuongeza Sh 2 katika ushuru wa bidhaa ya dizeli, na hivyo dizeli itaendelea na ushuru wa mwaka huu wa fedha unaoisha Juni 30, mwaka huu wa Sh 215.

Mafuta ya taa pia, ushuru uliokuwepo ulikuwa Sh 430 na Serikali wakati wa mvutano ilitaka uongezwe uwe Sh 475, lakini katika muafaka sasa utateremka mpaka Sh 425, na bado utasaidia kuzuia uchakachuaji wa mafuta, kwa kuwa utakuwa juu kuliko wa dizeli.

Hata hivyo, katika ushuru wa barabara unaotozwa katika petroli na dizeli, walikubaliana katika petroli uongezwe kutoka Sh 200, hadi Sh 263 na katika dizeli kutoka Sh 200 hadi Sh 263, ili barabara za vijijini zijengwe na nyingine zikarabatiwe.

Mgimwa alisema katika huduma za simu za kutuma na kupokea fedha, ushuru wa asilimia 14.5 uliokuwa uwekwe, sasa umeondolewa na utabaki katika kupiga simu, kutuma ujumbe mfupi na huduma zingine za simu.

Kodi ya magari yenye umri wa zaidi ya miaka 10, kwa magari ya kawaida kutoka asilimia 20-25 na katika magari ya kazi asilimia 5, Kamati ya Bunge pamoja na kuipinga, lakini ilikubaliana na msimamo wa Serikali.

Serikali pia imekubali kuchukua ushauri wa Bunge, wa kutafuta vyanzo mbadala vya mapato kutoka katika uvuvi wa samaki katika bahari kuu, uuzaji wa mashudu nje ya nchi na katika mashirika yenye tozo za moja kwa moja kutoka katika mafuta ya petroli.

Hata hivyo, Serikali ilikataa kuondoa Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (Tanapa) na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, katika kuwajibika kulipa asilimia 10 ya mapato ghafi yake au ya bajeti yake ya mwaka, katika Mfuko Mkuu wa Serikali kama mashirika mengine ya umma.


*Pinda, Makinda
Baada ya kumalizika kwa mvutano huo, Muswada wa Sheria ya Fedha ulipitishwa kwa ndio na wabunge wote bila kujali vyama vyao, huku Makinda akisifu kazi ya Kamati ya Bajeti, kwamba wanastahili kupata Phd ya heshima, kwani imeibadili Bajeti ya Serikali, huku Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, akisifu kuwa kazi nzuri imefanyika na kuisha salama.

“Wote mtakumbuka tumeanza Mkutano huu kwa changamoto kubwa ya mabadiliko ya mzunguko mpya wa kuwasilisha Bajeti ya Serikali na pengine kulikuwepo hoja ya mashaka kuhusu ufanisi wake. 

“Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba tumefanya vizuri sana, wote ni mashahidi kwamba waheshimiwa wabunge wamejadili kwa kina na kutoa ushauri wao ambao kwa kiasi kikubwa umezingatiwa na Serikali,” alisema Pinda.

No comments: